Wazo la kubuniwa kwa Chama cha Kiswahili lilianzishwa mwaka wa 1997 katika Kongamano lililoandaliwa na Idara ya Kiswahili, Chuo Kikuu cha Moi. Lengo la kongamano hilo lilikuwa ni kutathmini iwapo kulikuwa na uwezekano wa kuwa na kongamano ambalo lingewaleta pamoja wataalam wa Kiswahili nchini Kenya. Katika Kongamano hilo, kamati iliundwa ili ifanye kazi na idara ya Kiswahili, Chuo Kikuu cha Kenyatta ambacho kilikubaliwa kiwe mwenyeji wa Kongamano katika mwaka uliofuatia, 1998. Kupitia kwa juhudi za kamati na idara ya Kiswahili, Chuo Kikuu cha Kenyatta kongamano lenye kauli mbiu Kiswahili katika Karne ya 21 liliandaliwa.
Kamati andalizi iliyoteuliwa wakati huo ilipewa jukumu la kusajili wanachama kwa ushirikiano na Chuo Kikuu cha Maseno ambacho kilikuwa kimependekezwa ili kuwa mwenyeji wa kongamano la mwaka uliofuata wa 1999. Maudhui ya kongamano hilo yalikuwa Mustakabali wa Utafiti wa Kiswahili. Kufikia wakati wa kongamano hilo, chama kilikuwa kimepiga hatua katika usajili wa wanachama wapya.
Azma ya chama hiki ilikwa kuanzisha jukwaa la wataalamu wa Kiswahili (wahadhiri na walimu wa Kiswahili) na wadau wengine ili kujenga jukwaa ambalo lingetumika kuboresha utaalamu na ubadilishanaji wa maarifa ya kitaaluma hasa kuhusiana na maendeleo ya Kiswahili na nafasi yake katika ujenzi wa taifa.
Uthabiti wa jukwaa hili ulikuwa katika imani kwamba Kiswahili hutekeleza majukumu muhimu katika maisha ya watumiaji wake, si katika Afrika Mashariki pekee, bali pia ulimwenguni kote. Lugha ya Kiswahili pia ilikuwa imeonekana kuwa na uwezo wa kuteuliwa ili kuwa lugha ya taifa ya Kenya pamoja na Kiingereza, jukumu ambalo Kiswahili kilikuwa tayari kimetekeleza kwa mwongo mmoja tangu mwaka wa 2010 katiba mpya ilipozinduliwa. Kwa kuongezea, kulikuwa pia na mapatano miongoni mwa wanachama kwamba chama kikuze lugha hii ya Kiswahili ili kuinua hadhi yake inayostahili kama lugha ya kukuza maendeleo ya taifa.
Mnamo mwaka wa 2000, Chama kiliandaa Kongamano mjini Mombasa ambapo kauli mbiu ilikuwa Kiswahili kwa Mahitaji Maalum. Utaratibu huu uliendelea hivyo na mwaka wa 2002, CHAKITA ikishirikiana na Chuo Kikuu cha Egerton ambapo idara ya Lugha na Isimu iliandaa kongamano lililokuwa na kauli mbiu Lugha na Utandawazi na baaadye mwaka wa 2003 kongamano lingine likafuatia lenye kauli mbiu Kiswahili na Mikondo ya Fikra. Makongamano mengine yaliyofuata ni kama yafuatayo: Nakuru (2006), Chuo Kikuu cha Moi (2007), Chuo Kikuu cha Nairobi (2009), Mombasa (2016), Chuo Kikuu cha Kibabii (2017), Chuo Kikuu cha Moi (2018), Chuo Kikuu cha Karatina (2019). Kongamano ambalo lingefanyika katika Chuo Kikuu cha Kabaraka mwaka wa 2020, halikufanyika kutokana na janga la COVID-19. Kongamano la 2021 litafanyika katika Kaunti ya Baringo (Kenya School of Government).
Kila mwaka Chama hutangaza rasmi makongamano. Aidha, huandaa kongamano moja ambapo wanachama hutaarifiwa kuhusu Wito wa Ikisiri kupitia kwa baruapepe na pia matangazo yanatanganzwa moja kwa moja kupitia tovuti rasmi ya chama, mitandao ya kijamii (kama ile whassap na nk). Malengo yatakuwa ni kuwafikia wataalamu wengi iwezekanavyo. Katika matangazo hayo, arifa muhimu zitatolewa kuhusu Kauli Mbiu, Mada, sehemu ya kongamano, ada ya ushiriki na makataa ya ikisiri na uandishi wa makala. Kadhalika, kutakuwepo arifa mbalimbali kuhusu makongamano ya awali ya Chama katika tovuti. Anwani maalumu ya mawasiliano itatolewa kwa ajili ya makongamano. Makongamano haya yanatarajiwa kulenga wapenzi na wataalamu wa Kiswahili. Pia, makataa hutolewa kwa wajumbe kutayarisha makala ambazo zitawasilishwa ili kuweza kushiriki kikamilifu katika makongamano hayo ya kila mwaka. Matukio muhimu yatatangazwa kupitia tovuti rasmi ya Chama. Chama kinakaribisha wajumbe kutoka Kenya na mataifa mengine ulimwenguni.
Ufuatao ni muhtasari makongamano ya CHAKITA pamoja na sehemu zilizofanyika:
Mwaka Mahali Mada Kuu
1997 Chuo Kikuu cha Moi Uzinduzi wa CHAKITA
1998 Chuo Kikuu cha Kenyatta Kiswahili katika Karne ya 21
1999 Chuo Kikuu cha Maseno Mustakabali wa Utafiti wa Kiswahili
2000 Fort Jesus Mombasa Lugha na Utamaduni
2001 Chuo Kikuu cha Laikipia Lugha na Utandawazi
2002 Fort Jesus Mombasa Kiswahili kwa Mahitaji Maalum
2003 Chuo Kikuu cha Nairobi Kiswahili na Mikondo ya Fikra
2004 Silver Springs Hotel Fasihi Simulizi ya Kiswahili
2005 Mombasa Kiswahili na Elimu Nchini Kenya
2006 Hoteli ya Kunste Nakuru Isimujamii ya Kiswahili
2007 Chuo Kikuu cha Moi Kiswahili na Masuala Ibuka
2008 Fort Jesus Mombasa Lugha, Utaifa na Utangamano
2009 Lenana Hotel-Nairobi Ukuzaji wa Kiswahili
2010 Chuo Kikuu cha Pwani Kiswahili Tafsiri na Ukalimani
2012 Chuo Kikuu cha Kenyatta Kiswahili, Utangamano na Maendeleo
2013 CUEA Kiswahili na Maendeleo
2014 Chuo Kikuu cha Rongo Kiswahili na Utandawazi
2016 RISSEA Mombasa
2017 Chuo Kikuu cha Kibabii
2018 Chuo Kikuu cha Moi Lugha na Fasihi Katika Mshikamano wa Kitaifa na Uwiano
2019 Chuo Kikuu cha Karatina Teknohama na Maendeleo Endele
Kupitia kwa makongamano hayo, Chama kimeweza kuchapisha vitabu ambavo vimeasidia katika kuendeleza taaluma ya Kiswahili na Isimu kwa ujumla. Aidha, machapisho hayo yamesidia katika kusambaza matokeo ya tafiti za kila mwaka kuhusu matumizi ya Kiswahili. Miongoni mwa machapisho hayo ni:
Machapisho haya ya msingi yalitokana na makongamnao ya CHAKITA ambapo mawazo hayo yalitokana na wataalam na wasomi wa Kiswahili. Mbali na kuendeleza masuala ya kiusomi na kitaaluma, chama kimekuwa kikijihusisha na maswala ya elimu ambapo kiliwasilisha maoni kwa Tume ya Koech (1999) ambayo ilikuwa ikitathmini mfumo wa Elimu wa 8-4-4. Hoja kuu ilikuwa, Kiswahili kilihitaji kuwa somo la lazima na la kutahiniwa katika viwango vya shule ya Msingi na Upili nchini Kenya.
Mwaka wa 2006, baina ya mwezi wa Juni and Septemba, Chama kiliandaa makongamano katika maeneo mbalimbali nchini Kenya ili kuwahamasisha walimu wa shule za upili kuhusu namna ya kuhusisha mbinu mpya katika lugha ya Kiswahili. Kwa kuongezea, baada ya kuanzishwa kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki, kwa namna moja au nyingine CHAKITA kilihusishwa. Mnamo Februari 2, 2016, kupitia kwa uongozi wa Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Kiswahili ya Afrika Mashariki (KAKAMA), CHAKITA kilikuwa mdau muhimu katika jopo lililokabidhiwa jukumu la kuangazia uwezekano wa kutathmini Itifaki ya Kamisheni ya Kiswahili Afrika Mashariki.
Kufikia sasa chama hiki kimewasajili wanachama wengi kutoka vyuo vikuu na wadau wengine wa Kiswahili. Pia, CHAKITA kimewajibika na kinaendelea kufanya hivyo kuhusu uendelezaji na ukuzaji Kiswahili nchini Kenya. Vilevile, wahadhiri wengi wamepandishwa cheo kwa sababu ya kuwa wanachama hai wa CHAKITA.
Uongozi wa CHAKITA
Viongozi wa Chama huteuliwa kutokana na Mkutano Mkuu unaofanyika kila mwaka. Kwa kawaida, uchaguzi hufanyika baada ya miaka miwili. Kila mwanachama huwa huru kuwania wadhifa wowote; anaweza kuwania baada ya kupendekezwa na mmoja wa wajumbe na kuidhinishwa na mwanachama mwingine mmoja. Wanaoteuliwa huwa ni wanachama ambao wametimiza masharti ya Chama kama vile ulipaji wa ada za mwaka. Kama viongozi huunda kamati tendaji ambayo hutekeleza majukumu muhimu ya Chama. Kunapotokea haja ya dharura mkutano maalum huandaliwa na Wanachama kuarifiwa kupitia kwa barua pepe au katika mikutano ya Chama. Muundo na nyadhifa za viongozi wa Chama ni ufuatao:
Orodha ya Viongozi: 2019-2021
Muliro
UANACHAMA WA CHAKITA
Aina za Uanachama
Kuna aina mbalimbali za uanachama kama inavyoelezwa katika Katiba ya Chama: uanachama binafsi, uanachama asasi, uanachama wa heshima, uanachama wa kudumu na uanachama shirikishi. Uanachama binafsi, ambao ndio unaotawala, utakuwa wa aina mbili:
Kujiunga
Ada ya kila Mwaka
Ada ya kila mwaka ni Ksh. 2,000/= kwa wanachama wa kawaida na Ksh. 1000/= kwa wanachama wanafunzi
Matangazo Muhimu ya Makongamano ya CHAKITA
Kila mwaka Chama hutangaza rasmi Kongamano. Aidha, huandaa kongamano moja ambapo wanachama huarifiwa Wito wa kutuma ikisiri kupitia kwa barua pepe na pia matangazo hutolewa moja kwa moja katika mitandao ya kijamii kwa malengo ya kufikia wataalamu wengi iwezekanavyo. Katika matangazo hayo kuna arifa kuhusu sehemu ya kongamano, ada ya ushiriki na makataa. Kadahalika, kuna arifa mbalimbali kuhusu makongamano ya awali. Makongamano ya CHAKITA hulenga wapenzi na wataalam wa Kiswahili. Wajumbe hualikwa na wanaweza kutayarisha makala ambazo zitawasilishwa au kushiriki kikamilifu katika makongamano hayo ya kila mwaka. Matukio yanayojiri hutangazwa katika tovuti ya Chama. Chama hukaribisha wajumbe kutoka Kenya na mataifa mengine ulimwenguni.
Tangazo
Kongamano la 2021 litafanyika katika Kaunti ya Baringo (Kenya School of Government), mjini Kabarnet
Jarida hili hutokea mara moja kwa mwaka (Novemba) na huchapisha makala ambazo hazijawahi kuchapishwa katika taaluma ya Lugha, Isimu na Fasihi ya Kiswahili na lugha nyingine za Kiafrika. Makala yasiyozingatia masharti yaliyowekwa na wahariri hayawezi kuchapishwa.